Sunday, 30 July 2017

MAAZIMIO YA TIMU YA REAL KIDS FC INAYOSHIRIKI LIGI MADARAJA YA VIJANA BAADA YA ZFA CENTRAL WILAYA YA MJINI KUFANYA VITENDO VYA DHARAU NA KUKIUKA KANUNI NA SHERIA MASHINDANO WALIZOZIWEKA WENYEWE

Ndugu waandishi wa habari…..
Viongozi wa Real Kids wakizungumza na waandishi wa habari.

Awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kumshukuru M/Mungu kwa kutujaalia uzima afya kuweza kukutana hapa leo hii kwa ajili ya kuzungumzia maazimio ya Kamati tendaji ya Timu ya Reak Kids FC kama kichwa cha habari kinavyoeleza hapo juu.

Uongozi wa Real kids fc ulipokea barua siku ya Jumanne tarehe 25/07/2017 saa 1:00 za usiku yenye Kumbukumbu nambari KMV/CL/WM/VOL-39 naomba kuisoma.

Baada ya kupokea barua hiyo Uongozi wa timu ya Real Kids fc tuliijadili kwa kina na kupinga maamuzi hayo kwa kuandika barua ya kukata rufaa ngazi husika na kumfikia Katibu wa Kamati Central Taifa barua ya tarehe 26/07/2017 yenye kumbukumbu nambari RKFC/26/2017 kabla ya masaa 48 kama inavyoeleza Kanuni kifungu cha 20 ©. “.." naomba kuisoma barua hiyo. Na nakala ya barua hiyo ilimfikia M/Kiti wa ZFA Central Wilaya ya Mjini siku ya Alhamis ya tarehe 27/07/2017 saa 12:06 za jioni.

Kwa vile Timu ya Real Kids fc ilikua imeingia fainali ya ligi ya mtoano tulitegemea kwamba Kamati itasitisha zoezi la utoaji zawadi kwa bingwa ligi ya mtoano daraja la Central mpaka pale rufaa yetu itakaposikilizwa na kutolewa maamuzi.

Kabla ya kuelezea maazimio yetu naomba kutoa udhaifu wa aliyejipa mamlaka ya kutufuta kwenye mashindano kwa kutumia chuki zisizokua na msingi'

1. M/Kiti wa ZFA Central Wilaya ya Mjini Ndg. Khamis Machano alidiriki kudanganya na kwa kukiuka maamuzi ya kamati yake kwa kuitetea timu ya Mapembeani katika kesi ambayo tayari ilikua imeshatolewa hukumu na kamati yake.

2. Kuwaondosha FC Mwembebeni katika ligi ya mtoano na kuwaachia waendelee kushiriki ligi kwa kuchelewa kwao kulipa ada ya mashindano. ( wakati huo huo Real Kids fc kuondolewa kabisa ligi zote mbili )

3. Kusitisha kuchezwa kwa fainali ligi ya mtooano ambayo ilitakiwa kuchezwa kabla ya mfungo wa mwezi wa ramadhani kwa kusubiria kesi ya Timu ya Mapembeani FC ambayo ilikata rufaa ngazi ya juu kutolewa maamuzi. (Kudharau rufaa ya Real Kids fc)

4. Kufumbia macho mambo ya kishirikina yanayofanywa wazi wazi na baadhi ya timu na kukiuka kifungu cha 26 a(i) na (ii) kinachozungumzia Imani za kishirikina na uchawi.

Baada ya ZFA Central Wilaya ya Mjini kukabidhi zawadi za mshindi wa ligi ya mtoano kwa timu husika, Uongozi wa Real Kids fc ulikaa na kujadili kwa kina kitendo hicho cha ZFA Central Wilaya ya Mjini kwa kuonesha dharau na kukikuka kwa makusudi kanuni na sheria walizozeweka wenyewe. Uongozi umefikia maazimio yafutayo;-

1. Tunalaani vikali hatua ya ZFA Central Wilaya ya Mjini kuendelea kutumia nguvu ya madaraka yake kutoa maamuzi bila kuzingatia sheria na taratibu walizoziweka wenyewe katika kanuni yao ya kuendesha mashindano.

2. Tunaendelea kupinga kile kinachoitwa kufanya vitendo vya utovu wa nidhamu na kupanga matokeo katika mchezo wetu dhidi ya FC Mwembebeni kama ilivyoelezwa katika barua yao niliyoisoma hapo awali.

3. Tunalaani vikali vyombo vya habari pamoja na magazeti yote yanayoendelea kuchafua jina la timu yetu kupitia kwa kauli za M/Kiti wa ZFA Central Wilaya ya mjini bila ya kuzifatilia, kuzihakiki na kuthibitishwa na pande zote zinazohusika kwa kile wanachodai kua tumefanya kitendo cha utovu wa nidhamu na kupanga matokeo. Kuendelea kutoa habari hizi ni kuenda kinyume na sheria za nchi na Real Kids Fc haitosita kuwafikisha kwa vyombo husika ili kila mwandishi anaendelea kuchafua jina letu kuchukuliwa hatua za kinidhamu kama sheria za nchi zinavyoagiza.

Tunapenda kutoa wito.       

1. Tunawaomba waandishi wa habari pamoja na wahariri wa magazeti kufatilia kwa kina habari zote wanazozikusanya na wasikubali kujaribu kutuma habari kwa kuridhisha upande mmoja bila kujali ukubwa na wadhifa wa mtu husika kwa kufanya hivyo kutaweza kumuweka hatiani kama sheria ya nchi inavyoagiza.

2. Tunaomba Waziri wa wizara husika aliyepewa dhamana ya kusimamia michezo awaangalie vijana kwa jicho la huruma kwani viongozi waliopewa dhamana ya kuwasimamia wanawakandamiza kwa kutumia mwemvuli wa kanuni na kujali maslahi yao binafsi na kusahau dhamna kubwa ya kukuza na kundeleza vipaji vya vijana waliyopewa.

3. Tunamuomba M/Kiti wa Central Wilaya ya Mjini Ndg. Khamis Machano atoke kwenye vyombo vya habari akubali kukiuka kanuni za mashindano kwa kupokea nakala ya rufaa ya timu ya Real Kids fc na kuidharau kwa makusudi na awajibike kisheria kwa kujiuzulu kwa kushindwa kwake kusimamia kanuni na sheria za mashindano walizozipanga wenyewe.

4. Tunaiomba kamati husika inayochagua viongozi wa madaraja ya vijana kuweka sheria ya kuwachagua viongozi wanaotuongoza kwa kuwapigia kura ambayo watashirikishwa viongozi wa vilabu vyote husika kwani kufanya hivyo kunaweza ndio kutaweza kuleta viongozi imara wenye kuwatumikia vijana wetu.

Mwisho napenda nichukue fursa kuwaomba wadau wetu wa real kids fc kutulia na kuendelea kutuunga mkono sambamba na kupuuza kile kinachodaiwa kufanya vitendo vya utovu wa nidhamu na kupanga matokeo, Ungozi wa Timu ya Real Kids fc upo imara na hauwezi kuyumbishwa na kauli hizo za kuchafuliwa kwa jina letu.

Ahsanteni kwa kunisikiliza….

IMETOLEWA NA
KAMATI TENDAJI
REAL KIDS FC
30/07/2017

No comments:

Post a Comment